Janga la Yanga si la Kitoto

 Picha
JANGA linaonekana kuendelea kuwakabili wawakilishi pekee wa Tanzania kwenye michuano ya kimataifa, Yanga yenye maskani yake Jangwani, Dar es Salaam.
Yanga ambao kwa sasa wanaonekana kutokuwa sawa kiuchumi na kiuongozi pia wamekuwa hawapati matokeo mazuri katika mechi zao za kimataifa. Mabingwa hao wa msimu wa mwaka 2016/17 walipata tiketi ya kuiwakilisha nchi mwaka huu kwenye michuano ya kimataifa wakishiriki Ligi ya Mabingwa Afrika. Mambo hayakuwa mazuri kwao kwani walishindwa kuhimili vishindo vya wababe waliokutana nao kwenye michuano hiyo na kujikuta wakitolewa hatua ya kwanza.
Kutokana na kufika hatua hiyo kanuni ya Shirikisho la Soka Afrika (Caf) inayosimamia michuano hiyo ikawaruhusu kuangukia kwenye hatua ya mtoano ya Kombe la Shirikisho Afrika ambapo huko walipambana hadi wakafanikiwa kuvuka hatua hiyo mpaka kwenye makundi. Kwenye makundi wamepangwa kundi D pamoja na timu za USM Alger ya Algeria, Rayon Sports ya Rwanda pamoja na Gor Mahia ya Kenya.
Kwenye hatua hiyo napo hali si hali kwani kwenye mechi tatu walizocheza mpaka sasa wamejikuta wakiburuza mkia wakiwa na pointi moja tu huku USM Alger wakiongoza baada ya kupata pointi saba kwenye michezo yao mitatu, Gor Mahia wenye pointi tano wanashika nafasi ya pili na ya tatu inakamatwa na Rayon Sports ambao wenye pointi mbili. Washindi wawili wa kundi ndio watavuka hatua hiyo na kwenda robo fainali hali inayoonekana kuwa ngumu kwa Yanga kuvuka hapo.
Hesabu ambazo zitawabeba Yanga mpaka hatua inayofuata ni kuwa wanatakiwa washinde mechi zote tatu ambazo zitawafanya wafikishe pointi 10 huku wakiombea mmoja kati ya timu walizonazo kwenye kundi hilo ashinde mechi mbili zilizobakia. Kama USM Alger watashinda mechi mbili na kupoteza ya Yanga watafikisha pointi 13 ambazo zitawafanya wavuke moja kwa moja.
Rayon ikishinda mechi mbili na kupoteza ya Yanga itafikisha pointi nane ambazo zitaifanya ivuke na Yanga. Gor Mahia kama wakishinda mechi mbili na kupoteza ya Yanga watafikisha pointi 11 ambazo zitawavusha yeye na Yanga. Kuna hesabu tofauti na hizo ambazo zinaivusha Yanga kwenye hatua hii lakini ni kwenye karatasi tu zinaonekana kuwa ni rahisi kukupa majibu lakini ni ngumu kwenye dakika 90 kutokana na kila timu kujipanga kivyake kuhakikisha kwenye raundi hii ya lala salama hawapotezi mchezo wowote kirahisi.
Mpaka sasa Yanga wameshacheza mechi tisa, kwenye michezo yote hiyo wamevuna pointi tisa tu, wameshinda mbili, wamefungwa nne na sare tatu. Safari ya Yanga ilikuwa hivi kimataifa Februari 10, 2018 Tarehe hiyo walikuwa na kibarua cha hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika, wakashuka kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, kucheza na Saint Louis na wakaibuka na ushindi wa bao 1-0 lililofungwa na Juma Mahadhi dakika ya 67 na waliporudiana kwenye Uwanja wa Linite, Victoria visiwani Shelisheli walitoka sare ya kufungana bao 1-1.
Machi 6, 2018 Baada ya matokeo hayo wakavuka mpaka hatua ya kwanza ambapo walikutana na Township Rollers wababe kutoka Botswana. Hapa wakakwaa kisiki baada ya mchezo wa kwanza hapa Dar es Salaam kukubali kipigo cha mabao 2-1 Machi 17, 2018 Tarehe hiyo timu hizi zilicheza mechi yao ya marudiano mjini Gaborone, wakatoka suluhu na kuwafanya watolewe kwenye michuano hiyo na kuangukia Kombe la Shirikisho. Aprili 7, 2018 Baada ya kuangukia kwenye Kombe la Shirikisho wakapangiwa kukutana na Welayta Dicha kutoka Djibout.
Kwenye mchezo wa kwanza walijitutumua na kuibuka na ushindi wa 2-0. Aprili 18, 2018 Wakarudiana na Dicha na hapa Yanga wakafungwa 1-0 lakini matokeo haya hayakuwanyima nafasi ya kutinga hatua ya makundi. Mei6, 2018 Walicheza mchezo wao wa kwanza na USM Alger mjini Algiers kwenye Uwanja wa 5 Juilete 1862 na kukubali kipigo cha mabao 4-0. Mei 16, 2018 Wakiwa kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakashindwa kupata pointi tatu mbele ya Rayon Sports baada ya kumaliza dakika 90 suluhu. Julai 18, 2018 Wakiwa Uwanja wa Moi, Nairobi, Kenya wakakumbwa na kipigo kingine cha mabao 4-0 ukiwa ni muendelezo wa matokeo mabaya kwa klabu hiyo.
Kazi ngumu inausubiri Yanga mbele ili kusonga mbele, ama imalize hatua ya makundi na kujipanga na msimu mwingine wa ligi.

Comments

Popular posts from this blog

Mwinyi aongoza maziko ya baba mkwe wa Kikwete

HII NI NEEMA KWA MRISHO MPOTO